Kwa mujibu wa taarifa ya Shirika la Habari la Hawza kutoka Tehran, Jenerali Mahamadou Sana, Waziri wa Usalama wa Burkina Faso, akiwa na ujumbe wa ngazi ya juu kutoka nchi hiyo, alitembelea sehemu mbalimbali za Makumbusho ya Kitaifa ya Mapinduzi ya Kiislamu na Vita vitakatifu vya Kujihami.
Ziara hiyo ililenga kujifunza kuhusu simulizi sahihi na za kihistoria za Mapinduzi ya Kiislamu na Vita vya Kujihami Vitakatifu, pamoja na mifano ya mapambano ya wananchi.
Mwanzoni mwa ziara hiyo, Sardar Mahdi Amirian, Mkurugenzi Mkuu wa makumbusho hayo, alimkaribisha Waziri na ujumbe wake, akitoa maelezo kuhusu historia ya kuanzishwa kwa makumbusho hayo, malengo yake ya kielimu na kitamaduni, pamoja na nafasi ya msingi ya wananchi wa Iran katika kipindi cha vita vya kujihami.
Baadaye, wageni kutoka Afrika walitembelea kumbi nane za makumbusho hayo na kufahamu matukio yaliyosababisha ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu, Vita vya Kulazimishwa, na maendeleo yaliyofikiwa baada ya hapo.
Jenerali Mahamadou Sana, Waziri wa Usalama wa Burkina Faso, katika mahojiano kando ya ziara hiyo alisema: “Kile tulichokiona leo katika makumbusho haya kinaonesha imani, kujitolea, na mshikamano wa wananchi waliosimama imara kutetea thamani na uhuru wao. Uzoefu huu ni wa kufundisha na wa kuhamasisha sana kwetu.”
Akaongeza kusema: “Wananchi wa Iran wameonesha kwamba usalama wa kudumu hupatikana tu kupitia imani, umoja, na imani kwa malengo ya kitaifa. Huu ni mfano ambao mataifa mengine yanaweza kujifunza na kunufaika nao.”
Aidha, Waziri huyo alisisitiza juu ya utajiri wa kiutamaduni na kisanii wa kazi zilizomo katika makumbusho hayo, akisema: “Makumbusho haya hayaelezi tu historia ya taifa la Iran, bali pia yanabeba ujumbe wa kimataifa wa amani, mapambano, na heshima ya mwanadamu. Bila shaka, uzoefu wa wananchi wa Iran katika kulinda uhuru na usalama wao ni wenye thamani kubwa na unafaa kuigwa.”
Mwishoni mwa ziara hiyo, Waziri wa Usalama wa Burkina Faso alishukuru kwa ukarimu wa Mkurugenzi Mkuu na wafanyakazi wa makumbusho, na akaashiria kwamba; ushirikiano wa kielimu na kitamaduni kati ya mataifa hayo mawili utaimarika zaidi katika siku zijazo.
Maoni yako